MARA
nyingi tunapofikiria namna ya kumpata mwenza sahihi, huwa tunaangalia
ishu ya kumpata yule mwenye mapenzi ya dhati lakini kumjua anayekupenda
kwa dhati ni vigumu sana.
Ndiyo maana hapa chini nimekupa vigezo saba
vya mtu anayekupenda kwa dhati na anafaa kuwa mwenza wako endapo
mtakuwa tayari mmeshaanzisha uhusiano wa kawaida.
Mguso wa hisia
Hakika
mapenzi ni mguso wa hisia, kwa maana hiyo kigezo kikuu cha kuzingatia
kwa mtu anayestahili kuwa mwenzi wako wa ndoa ni vile ambavyo hisia zake
umeziteka. Hali kadhalika na wewe mwenyewe ulivyotekwa naye.
Amani
na furaha vikitawala kati yenu unajiona upo huru kwa kila kitu na
mnapokuwa hamuelewani kila kitu kwenye akili yako unaona hakiendi. Vivyo
hivyo na yeye kwamba amani ipo pale mnapoelewana na inatoweka
mnapokosana. Huyo ni wazi mnaendana.
Kutosheka
Ukiwa naye
unajisikiaje? Umetosheka eeh? Akiwa mbali inakuaje, unahisi kuna
upungufu mkubwa? Vipi na yeye anajiona hivyo hivyo? Kama jibu ni ndiyo
maana yake mnaendana kwa sababu ukamili wako unamtegemea yeye, hali
kadhalika na yeye.Anakata kiu yako yote? Na upande wake inakuaje? Ikiwa
ni hivyo, basi anatosha kuwa mwenzi wako wa maisha.
Malengo
Kila
mtu anapoingia kwenye uhusiano wa kimapenzi, lengo lake huwa ni kudumu.
Achana na hulka za viruka njia. Pointi hii inakujenga kujua matarajio
ya mwenzako kuhusu wewe. Anakuhitaji kwa maisha yake yote au yupo na
wewe kwa sababu hana pa kwenda?
Wengi wapo kwenye majuto kwa sababu
waliingia kwenye ndoa na watu ambao hawakuwa na nia ya dhati nao, bali
walijichanganya baada ya kukosa uelekeo.
Ishu ya mawasiliano
Anapenda
kuwasiliana na wewe, ukimtumia SMS anaijibu ‘fasta’. Hatengenezi sababu
ya kutowasiliana na wewe, daima anaona njia pekee ya kuwaweka karibu
hata kama mpo mbali ni kuwasiliana. Nawe unampigia simu kwa wakati,
unasikia raha kupokea ujumbe wake naye anaona fahari kupigiwa simu na
wewe.Kama hali hiyo ipo, basi upendo wa kweli upo na hiyo inatosha
kuthibitisha kwamba mnaendana. Ukituma SMS naye akachelewa kujibu ni
wazi haoni umuhimu wako.
Ni wa shida na raha
Hapa ni hisia tu,
ikiwa mnapendana kwa dhati basi akiumia nawe yatakuwa ni maumivu yako.
Ikiwa hauna raha halafu yeye ni mwenye furaha basi huyo anakupenda
kinafiki. Hatofautiani na yule anayebembeleza ndoa ili kuondoa mkosi.
Kuwa makini, hakikisha unakuwa na mtu ambaye ni wa shida na raha.
Anajuta na kuomba msamaha
Mpenzi
bora ni yule anayejutia kosa pale anapokukosea, pia anaomba msamaha.
Hapa ieleweke kuwa kuomba msamaha peke yake haitoshi, isipokuwa anapaswa
kuonesha wazi kwamba ametambua makosa yake na amejuta.
Kimsingi mtu
mwenye sifa hiyo huwa hasumbui mnapokuwa ndani. Epuka mtu mbishi,
anakosea na hatambui kosa lake na badala yake anajenga hoja.
Hayuko tayari kukukosa
Mnagombana
anaumia lakini bado yupo na wewe. Anakuonesha waziwazi kuwa hayupo
tayari kuachana nawe. Yupo radhi kutumia muda mwingi kutafuta suluhu ili
muendelee kuwa pamoja. Hiyo inaonesha kuwa anakupenda kwa dhati.
Mtu
mwenye moyo mgumu, mnagombana wala hashtuki na hatengenezi mazingira ya
kurudiana, maana yake hana hisia za kweli, na anavyokuchukulia ni
kwamba hata mkiachana yeye anaona sawa.
Jiangalie na wewe!
Umeangalia
yote hayo, sasa jiangalie na wewe mwenye. Moyo wako unakusukuma kuwa na
yeye? Hilo ndilo swali la msingi kwa sababu mapenzi hayataki majaribio,
ukiingia ndiyo imetoka. Yanini kujipa kumbukumbu mbaya baadaye.
Maisha
bora au mabaya ya baadaye yanatokana na uamuzi wa leo, mwenzi sahihi wa
maisha ni mbolea ya furaha ya kudumu baadaye. Kwa hiyo kabla hujaingia
kwenye uhusiano wa ndoa ni vema kujiuliza mara mbilimbili.